Ni Siri Kuu - The Great Mystery

Ni Siri Kuu - The Great Mystery
"Wakati ule Yesu akajibu, akasema, Nakushukuru, Baba, Bwana wa mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya uliwaficha wenye hekima na akili, ukawafunulia watoto wachanga. Naam, Baba, kwa kuwa ndivyo ilivyopendeza mbele zako.

Alhamisi, 28 Agosti 2014

WAJUA KUWA WE NI MFALME NA KUHANI!

kongamano la Maombi ya Shule na Masomo

Na Goodluck Kazili

UMENUNULIWA NA KUFANYWA KUWA UFALME NA KUHANI KWA MUNGU KATIKA NCHI
 
Si hadithi wala simulizi, bali ni kweli na hakika kuwa Kristo alichinjwa akawanunua watu wa kila kabila , lugha, jamaa, na taifa na akawafanya kuwa ufalme na makuhani wanamiliki juu ya nchi.
Si tu bahati kupata nafasi ya kusoma na kusikia habari hii, bali pia ni neema ya MUNGU kwako, hivyo nakusihi kwa upendo wake Yeye aliyetuumba uzitafakali habari hizi kwa kina nazo zitakufaa na kukusaidia kwa wakati wake.
Kwa msaada wa Roho Mtakatifu nalipenda nikushirikishe habari za nafasi yako kwa MUNGU, katika kanisa, katika nchi/taifa au jamii na familia yako. Si rahisi kujua nafasi yako, lakini imekupasa kuifikiria kwa kuwa hakuna atakayefikri kwa ajiri yako bali ni wewe mwenyewe.
Iko nafasi mhimu na kubwa mbele za MUNGU uliyo nayo, hivyohivyo ulivyo, japo nyumbani wanaweza wakawa wanakudharau na kukuona kuwa si lolote. Lakini mimi leo kama sauti ya MUNGU kwako jijue kuwa una nafasi kubwa na ya heshima mbele za MUNGU. Na nafasi hiyo ni ya mhimu sana kwako . haijalishi una maisha ya dhambi kiasi gani, lakini bado MUNGU ni m,wema kwako, maana maandiko yanasema “Tena zitokazo kwa Yesu Kristo shahidi aliye mwaminifu, mzaliwa wa kwanza wa waliokufa na mkuu wa wafalme wa dunia. "Yeye atupendaye na kutuosha dhambi zetu katika damu yake. Na kutufanya kuwa ufalme na makuhani wa MUNGU, naye ni Baba yake ; utukufu na ukuu una Yeye hata milele na milele amina”. (ufunuo 1:5-6)
Mpendwa katika Kiristo Yesu, nakusihi kwa neema hii; basi ujitahidi kumpenda MUNGU na kutafuta sana kumjua Yeye ili kwa msaada wake maisha yaweze kukamilika. Maana hakuna maana ya maisha pasipo MUNGU mwenye kuyafanya maisha. Na kwa kuwa sisi tuliompokea Kristo tulifanyika kuwa watoto wa MUNGU, basi imetupasa kuyatambua haya ya kuwa yapo kwa ajiri yetu.
Ni mhimu kukumbuka kuwa, jambo lililo jema huja kwa wakati wake, basi hakika hili ni jambo jema. Kwa kuwa kama ungelijua tangu hapo kuwa wewe ni kuhani juu ya nchi katika ufalme wa MUNGU, basi pengine ungekuwa na hatua kubwa. Hata hivyo nakukumbusha kuwa hakuna wakati utakao kuwa mwema kwako zaidi ya wakati huu.
Hivyo nakusihi ufikiri kama mtu mhimu, ambaye anategemewa sehemu nyingi na watu wengi.  Tena maneno haya usiyasahau, elimu ipo ili kukupa maarifa, na kwa kuwa kuna namna mbili, basi ni mhimu kuwa na maarifa ya pande zote, kwa kuwa unaishi pande zote. Ni hatari sana kutokuwa na maarifa juu ya nmna hizi mbili.
Kwa hakika yapo maarifa ya roho na yapo maarifa ya mwili. Maarifa haya yote ni mhimu sana kwako, japo maarifa ya roho yanaonekana kuwa na thamani kubwa. Yanaonekana ya thamani kwa kuwa si wengi wanaobahatika kuyapata, kwa sababu hawayatafuti. Sasa sikushauri wewe ujaribu kutoyatafuta, itakuwa hatari sana. Tafuta maairfa ya roho na haya ya mwili kwa kuwa yote yatakusaidia katika maisha yako yote ya sasa na ya badae, hata baada ya kufa.
Ningeweza kukuandikia mengi, lakini kwa ufupi huu, naomba utafakari sana jinsi unavyowaza na unavyoenenda, je namna hiyo itakusaidia kufika hapo alipokukusudia MUNGU? Ikiwa ni ndiyo MUNGU akutie nguvu katika juhudi hizo, na ikiwa siyo basi MUNGU  akusaidie ili ujitahidi kwa dhati kuubadili mwenendo na mawazo yako. Uyatambue haya kuwa yamekujia kwa wakati sahihi wa wewe kubadilika na kuanza kufikri sawasawa na makusudi ya MUNGU aliyekuumba. Usipoteze muda ni wakati wako maana “ Nao waimba wimbo mpya wakisema wastahili kukitwaa hicho kitabu na kuzifungua mhuri zake,kwa kuwa ulichinjwa ukamnunulia MUNGU kwa damu yako watu wa kila kabila na lugha na jamaa na taifa, ukawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu; nao wanamiliki juu ya nchi” ufunuo 5:9-10
Haya ndiyo nalipenda nikushirikishe japo kwa ufupi, MUNGU akubariki .
Goodluck Kazili  0765-129960

SIRAHA MOJA MHIMU YA VITA YA KIROHO



KUHANI GOSPEL TEAM (KGT)TANZANIA)



SIRAHA MHIMU ZA UFALME WA MUNGU

Linapotajwa Neno siraha, kuna kitu kinajengeka ndani yako, na wakati mwingine utapata picha fulani. Hata hivyo suala la siraha lipo ikiwa tu kuna vita au ulinzi au uharibifu. Kama ilivyo katika mwili pia katika ulimwengu wa roho  zipo siraha, na zinamatumizi mbalimbali.

Mpendwa katika Kristo, ni wazi kuwa, siraha hizi za ufalme wa Mungu, ni mhimu kuzijua zote pamoja na matumizi yake, lakini pia umhimu wake.
Waefeso 6:10, inaeleza kuwa tuzidi kuwa hodari katika uweza wa Mungu na nguvu zake, lakini anasema uhodari wetu upo kwa kuzivaa siraha zote za MUNGU. Hapa unagundua kuwa zipo siraha nyingi za MUNGU, na ikiwa zipo nyingi zaidi ya moja kama maandiko yanavyothibitisha, basi ni hakika kuwa, zinatofautiana katika matumizi pia.

MUNGU alipotengeneza siraha tofauti tofauti, alikuwa na maana kubwa, na siraha hizo hutumika kwa wanadamu tu na zipo zitumikazo kwa malaika, ila hatutazungumzia hizo za malaika ila tutazungumzia zilizowekwa kutumiwa na wanadamu au duniani. Kama nilivyoeleza kuwa siraha hizo zinatofautiana kwa namna nyingi.


Mtumiaji wa siraha
Huyu ni mtu mhimu sana kwa kuwa siraha za Mungu zilizotengenezwa kwa ajili ya wana wa ufalme wa MUNGU hapa duniani, haziwezi fanya kazi hadi awepo mtumiaji, na kama mtumiaji atakosa maarifa basi siraha hizo zitafanya kazi kwa kiwango cha maarifa alichonacho mtumiaji.

AINA ZA SIRAHA ZA UFALME WA MUNGU

SIRAHA YA IMANI
Hii ni siraha ya kwanza, si kwa ukubwa ila inayobeba siraha nyingine pia. Kwa mjibu wa waebrania 11:1 imani ni kuwa na hakika), si kitu cha kubahatisha, ila ni uhakika ambao mtu anakuwa nao juu ya jambo Fulani, tena jambo hilo lisiwe la wakati huo ila liwe la wakati ujao na lazima liwe halionekani. Ukisikia kitu kisichoonekana ina maana kuwa kitu hicho ni cha kiroho.

Kwa maana nyingine tunaweza kusema, imani ni namna ya roho inayosimama kama nguvu, siraha, mamlaka, uwezo, uhakika na kuamini, inayotarajia kutekeleza au kutekelezwa kwa jambo fulani. Kwa msingi huo imani si kuamini tu kuwa Mungu anaweza ila ni zaidi ya kumwamini MUNGU.  Mwili una kawaida ya kutokuamini vitu vya rohoni, hivyo wakati mwingine mwili unaweza kukutia moyo kuwa Mungu anaweza kila kitu ila ikifika kwenye tatizo mwili utakuambia hili siyo la kawaida. Lengo la kukuambia hivyo ni ili kukuondoa kwenye imani halisi ya utendaji ambayo ndiyo kubwa.

Kuna imani ya kumwamini Mungu kuwa anaweza, lakini pia kuna imani zaidi ya kumwamini Mungu kuwa anaweza. Ukweli ni kuwa kitendo cha kumwamini Mungu kuwa anaweza ni hatua ya kwanza ya imani, kuishia hapo hakuwezi kusaidia kitu zaidi ya kuwa na tumaini tu, lakini ukitaka kuiona, imani ikifanya kazi yake, lazima kuamini huko ukufanye kuwa kitendo.

Mfano mama hana mtoto, na ameomba na kuhitaji sana kupata mtoto na hajapata, kwa hakika ni kuwa mama huyo anaweza akawa anamwamini Mungu lakini kumwamini Mungu huko hakuwezi kumsaidia asilimia nyingi kupata mtoto, isipokuwa kinachoweza kumsaidia ni pale anapoweza kubadili ile hali ya kuamini, iwe tendo.

Mfano mama anaweza kuamua na kusema, kwa kuwa imani ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo na ni yale mambo yasiyoonekana, hivyo basi itampasa kuwa na uhakika ndani kuwa, mwakani atakuwa na mtoto na inampasa kufanya maandalizi  kwa kuanza kununua vifaa vyote vya mtoto atakayemzaa, na wakati huo pengine hata mimbabado.  Mungu akiiona imani hiyo hakika lazima amfanyie mama huyo hata kama mpango haukuwepo.

Ukisoma maandiko matakatifu, unagundua kuwa wakati Yesu alipokuwa akiendelea na huduma kati ya vitu alivyokuwa anaangalia ilikuwa imani ya mtu, wakati mwingine hata kama mtu alikuwa hasitahili kutendewa lakini kwa imani yake ilimulazimu Yesu kumfanyia haja yake.

Nakuomba usome kwa umakini mistari hii uione imani jinsi ilivyo na hapa ndipo Roho alipokusudia kukufundishia suala la imani
“(Mathayo 15:22-28), Natazama, mwanamke mkananayo wa mipaka ile akatokea, akampazia sauti akisema, unirehemu, Bwana, mwana wa Daud; binti yangu amepagawa sana na mapepo. 23 Wala Yeye hakumjibu neno. nao wanafunzi wake wakamwendea, wakamwomba, wakisema mwache aende zake; maana anapiga kelele nyuma yetu.  24 Akajibu, akasema, sikutumwa ila kwa kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.    25 Naye akaja akamsujudia, akasema Bwana, unisaidie. 26 Akajibu, akasema, si vema kukitwaa chakula cha watoto na kuwatupia mbwa. 27 Akasema, Ndiyo, Bwana, lakini hata mbwa hula makombo yaangukayo mezani pa bwana zao. 28 Ndipo Yesu akajibu, akamwambia, mama imani yako ni kubwa; na iwe kwako kama utakavyo. Akapona binti yake tangu saa ile”

Sijui umepata kitu gani, lakini kwa kweli huwezi kuielewa imani vema hadi umeyapima mazingira na mazungumzo ya huyu mama na Yesu. Maneno yaliyolazwa ni kauli za mama mkananyo, maneno yaliyokolezwa na hayajalazwa ni ya Yesu mwenyewe na mengine walisema wanafunzi.

 Kama umefuatilia kwa nia ya kuijua imani sawasawa ni kuwa umegundua, yule mama alikuwa na mambo mawili makubwa, kwanza alikuwa na msimamo pili alikuwa na uhakika na anachokiomba majibu yake yapo. Uhakika ulimpa msimamo na msimamo ulimsaidia kulinda imani na kupata alichokuwa anakihitaji.
Jambo la ajabu, ni majibu ya Yesu, mstari wa 26 aliposema kuwa chakula alichonacho ni kwa ajili ya watoto wake na siyo kwa ajili ya mbwa, kwa lugha nyingine alimuita yule mama kuwa ni kama mbwa kwake. Hivi mfano wewe ukamwendea Yesu na kumsihi ukimuomba, halafu akakujibu kuwa ana majibu ya maombi ya watoto wake tu na siyo mbwa; unaweza ukafanyaje. kwa haraka haraka, inaweza ikawa ndio mwanzo na mwisho habari zako na Yesu, maana kama umemwendea kwa kumsihi na ukitegemea atakusaidia halafu bado ni Mungu, lakini anakupa majibu ambayo hata mpagani mwanadamu asingekupa kama umemwendea kwa unyenyekevu kiasi hicho.

Lakini hebu mtazame mama yule kwa unyenyekevu anamkaribia Yesu na kusema “ndiyo Bwana” kisha akajenga hoja asiyoitegemea Yesu, ni kweli mimi ni mubwa na pengine sistahili kula chakula ulichoandalia watoto wako, “ lakini hata mbwa hula makombo yaangukayo mezani pa bwana zao” Yesu alishangaa sana, maneno ya mama huyo yalikuwa na maana hii; kwa kuwa sistahili kula chakula ulichowaandalia watoto wako kwa sababu  mimi ni mbwa wako na siyo mtoto wako, basi uniruhusu tu nile makombo yaliyoanguka mezani pako maana hiyo ni haki yangu kama mbwa wako.

Hii ndiyo imani halisi inayotakiwa kwa watu wa MUNGU, ni wazi kuwa hujawahi kujibiwa kama huyu mama alivyojibiwa na alivyokatishwa tamaa na Yesu mwenyewe, lakini kwa imani yake alisimama akasema nina hakika na ninatarajia kupokea kwa namna yeyote. Na alipojenga msimamo huo Yesu akamtazama akasema Mama imani yako ni kubwa, na iwe kwako kama utakavyo, akapona binti yake tangu saa ile.

Ukisoma kwa kutafakari, na kwa undani unagundua kuwa, Yesu hakumuombea Yule mama juu ya mtoto wake, ila alimwambia iwe kwako kama utakavyo. Hebu fikri kama yule mama angekuwa anataka awe tajiri mimi nakuambia saa ile ile yule mama angekuwa tajiri. Si kwa maombi sana kuwa alipata alichotaka ila kwa imani yake, maana kama ni kuomba aliomba vizuri tena kwa unyenyekevu mkubwa; kama umesoma vema yale maombi ya yule mama yalikuwa ya unyenyekevu sana kuliko ya kwako unayoyaomba, hebu yatazame “akampazia sauti akisema, unirehemu maana yake unihurumie Bwana, mwana wa Daudi, lakini Yesu hakumjibu neno. Wanafunzi walipomtazama yule mama wakamhurumia na wao wakamwendea Yesu wakamsaidia kuomba wakasema mwache aende zake, maana yake mtendee ili aende zake maana anaendelea kupaza sauti. Bado Yesu hakujali maombi ya mama yule hata kwa kubembelezwa na wanafunzi wake, na badala yake akwaambia hakuja kwa ajili ya yule mama ila kwa wana wa Israeli waliopotea. Mama hakurudi nyuma japo kwa maneno hayo ilimtosha kuishi hapohapo, ila ajabu kuu aliendelea pamoja na kwamba Yeye hata kujibiwa hakujibiwa, ila wanafunzi walimsaidia ili angalau ajibiwe, bado anajibiwa kuwa Yesu hakuja kwa ajili yake. kwa hiyo ilimaanisha kuwa asitegemee kuwa anaweza kutendewa chochote kama anavyoomba, kama ni kuondoka aondoke tu. Yule mama baada ya kuambiwa hivyo akasogea akamsujudu, kuonesha kuwa hata kama hukuja kwa ajili yangu ila mimi nakuamini, alipomsujudu akaomba tena akisema, Bwana unisaidie. Baada ya Yesu kuona huyu mama anang’ang’ania akasema maneno magumu sana ambayo sasa yule mama kama si imani kubwa aliyokuwa nayo angekufulu palepale.

Swali langu kwako ni hili; huyu mama ana utofauti gani na wewe? Je Yeye hakuwa mwanadamu kama wewe? Je Yeye hakuwa na haja kama wewe ulivyo na haja? Na je umewahi kuomba ukakatishwa taamaa angalau robo ya huyu mama? Umewahi kujibiwa majibu kama alivyojibiwa huyu mama?. kwa kujiuliza hivyo, angalia imani yako, utagundua huna imani, na ndicho chanzo cha kutokupata kile unachotakana kuomba.

Hebu ngoja nikuambie jambo moja hapa la ajabu ili uone imani inavyofanya kazi kwa mhitaji lakini pia kwa yule anayeombea. Mathayo 17:14-16 inaeleza kisa kimoja, “Nao walipoufikia mkutano, mtu mmoja akamjia, akampigia magoti akisema. Bwana umurehemu mwanangu, kwa kuwa anakifafa, na kuteswa vibaya; maana mara nyingi huanguka motoni, na mara nyingi majini. Nikamlete kwa wanafunzi wako, wasiweze kumponya.” Ukiendelea kusoma unaona Yesu akichukia kwa ajili ya yule mtu, na juu ya wanafunzi wa Yesu kwa kuwa hawakuwa na imani. Ila alipomaliza kuwasema aliamuru wamlete kwake kisha akakemea yule pepo akamtoka yule mtoto.  Wanafunzi wake walipoona hivyo, hawakulidhika wakamwendea  mstari wa 19 “kisha wale wanafunzi wakamwende Yesu kwa faragha wakasema mbona sisi hatukuweza kumtoa? 20 Yesu akawaambia, kwa sababu ya upungufu wa imani yenu, kwa maana, amini, nawaambia, mkiwa na imani kiasi cha punje ya haradali, mtauambia mlima huu, ondoka hapa uende kule, nao utaondoka; wala hakutakuwa neno lisilowezekana kwenu”

Naamini umeona kazi ya imani na jinsi imani ilivyo, ila ukisoma sehemu nyingine wanafunzi walipoambiwa hivyo waliomba waongezewe imani ndipo Yesu akawaambi mngelikuwa na imani hata chembe ya haradali , kwa maana kuwa hawakuwa na imani hata ndogo japo walikuwa ni wanafunzi wa Yesu na walikuwa wanamwamini Yesu. Hapo unagundua kuwa imani ni zaidi ya kumwamini Yesu, lakini pia amesema  hakutakuwa na neno lisilowezekana kwenu. Unafikri kwa nini mambo mengi hayawezekani kwako, ni kwa sababu huna imani japo unamwamini Mungu. Ni wazi kuwa ungekuwa unaweza ungeniuliza swali sasa hiyo imani ya zaidi ya kumwamini Mungu iko je? na ndio unafanya je?. Roho mtakatifu alijua kuwa utahitaji kujua na ameweka majibu ya maswali yako hapa chini. Ila nakusihi sana isiwe tu kusoma na kuelewa bali iwe kusoma na kutenda hicho unachogundua na kukielewa.

Ukisoma hapo kwenye mathayo 17 lakini mstari wa 21 umetoa majibu. “ lakini namna hii haitoki ila kwa kusali na kuomba” hapo humaanisha kuwa namana hiyo ya imani inayoweza kutoa nguvu za namna hiyo haiwezekani isipokuwa kwa kufunga na kuomba. Maana yake ni kuwa kuna kiwango cha imani unachoweza kukipata kwa kuamini na kufanya kile unachokiamini kiwe hakika na kutenda vile unavyoaamini, lakini kiwango halisi cha imani hupatikana kwa kufunga na kuomba.
Hii ni kwa sababu mwanadamu ana namna ya mwili sana kuliko namna ya roho na kwa kweli hakuna mahali popota ambapo mwili unakubali na kumruhusu mtu kuwa na imani hasa ya utendaji, hivyo kufunga maana yake ni kuutiisha mwili ili kupandisha ile nafasi ya roho, hivyo kumfanya mtu kuwa na hali ya roho kuliko ya mwili. Pia kufunga huko kunaudhoofisha mwili ambako kudhoofika huko huifanya roho kuwa na nguvu.

Pia kuomba hutifua au hunyanyu hali ya roho, au hunyanyua hali ya kimungu ndani ya mtu, na hupunguza kasi ya mwili kufikri kimwili na kuifanya akili ikae kwa namna ya roho ambapo ni rahisi sana kuwa na imani na kuona kuwa kila kitu kinawezekana kwa Mungu, na kwa kuwa unakuwa kwa namna ya roho zaidi utasikia msukumo ambao unakusukuma kufanya kile unachokiamini na unapofanya kwa kuwa unafanya kwa uhakika lazima kitokee.

Mpendwa katika Kristo, siraha ya imani ni siraha kubwa sana, na wakati mwingine imekupasa kufanya mazoezi ya imani, hata pale ambapo watu wote wanaona ni ngumu, wewe unawaambia inawezekana, pale akili yako inapokuambia hapa ni ngumu unalazimisha ikubali kuwa inawezekana hata kama kwa jinsi ya kawaida haiwezekani.

Kikubwa jitahidi kuamini, na kufanya kile unachokiamini kiwe kweli, yaani kama unaamini Mungu anaweza katika jambo Fulani weka uhakika, na kisha lifanye ikiwa unomba uambiwe omba ukijua nikimaliza kuomba nitakuwa nimepokea, na ukimaliza hata kama hujaona majibu anza kujiaminisha kuwa umepokea taratibu taratibu utaanza kusikia amani moyoni na kuona lile jambo likikamilika.

Mungu wa mbinguni akujalie kujua vema siraha za ufalme wake ili uwe askari mwema na mtetezi wa wokovu wako na kuujenga mwili wa Kristo. Hata hivyo ujue kuwa ziko siraha nyingine kama siraha ya Neno, Siraha ya Maombi, Siraha ya Wokovu. Hizo ndizo siraha kuu za ufalme wa Mungu. Na hata siraha hiyo ya imani imeelezwa kwa ufupi hivyo endelea kusoma kwenye maanidiko juu ya imani na vitabu vya Neno la Mungu, semina, mikutano, na zaidi shuhuda mbalimbali. Maana imani chanzo chake ni kusikia ambako huja kwa Neno la Kristo. Mungu wa mbinguni akujalie mema yote.

“mjue sana Mungu ili uwe na amani”

Mwl: Goodluck Kazili

Kunihusu

Picha yangu
"Wakati ule Yesu akajibu, akasema, Nakushukuru, Baba, Bwana wa mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya uliwaficha wenye hekima na akili, ukawafunulia watoto wachanga. Naam, baba , kwa kuwa ndivyo ilivyopendeza mbele zako. (Ni Siri Kuu)

Tafuta katika Blogu Hii